UJUMBE WA PRINCE AMOS



Katika siku hizi za mwisho Bwana atafanya kazi kwa namna iliyotofauti sana na vile watu walivyodhani. Itakua ni kinyume kabisa na akili ya mwanadamu na utaratibu wa kibinadamu. Sio kila mtu katika zama za zamani za Biblia aliitwa kufanya kazi na Taasisi (Mfumo) uliokuwepo. Ingawa walikuwepo walioitwa kufanya kazi ndani ya System (Kanisa) lakini kuna wengine walipewa kazi tofauti kabisa na Taasisi zilizokuwepo, na watu hao walipitia wakati mgumu sana, kwani watu waliokua kwenye "Mfumo" waliwapiga vita sana. Kwa mfano Yona alitumwa akahubiri injili Ninawi kitu kilichokua tofauti kabisa na utaratibu wa dini na kanisa Yona alilokua akisali. Kwani watu wa Ninawi walikua wakichukiwa sana na Waizraeli, na Waizraeli waliamini kabisa kwamba     watu wa Ninawi wanastahili hukumu za Mungu, hawastahili kusikia habari za Mungu wa kweli, na kusogeleana nao ni kujitia unajisi. Yohana mbatizaji alipoitwa, alifanya kazi nnje kabisa na Kanisa la kiyahudi lililokuwepo. Na ndio maana wakuu wa dini hawakumwamini na ilifikia hatua wakatuma wapelelezi  kuchunguza alikotoka na amepewa kibali na nani!. Viongozi wa Kanisa la wayahudi walidhani kwamba wao tu ndio waliopaswa kumpa kibali Yohana cha kuhubiri. Na ilipaswa Yohana apitie kwanza kwenye shule zao. Ingawa Kanisa lililokuweko lilimkataa Yohana na utume wake, lakini Yohana kwa imani alitimiza kazi Mungu aliyompa na akalala kwa ushindi mkubwa sana. Sio rahisi hata kidogo kazi Bwana aliyonipa kueleweka kwa ndugu zangu wa Yerusalemu, Yesu aliponitokea "aliniambia wazi kwamba nitakutana na upinzani mkubwa sana, watu haswa walio kwenye mifumo ya kidini hawatanielewa, watanipiga vita sana, lakini nikivumilia hata mwisho nitakula matunda ya mti wa uzima na kuyanywa maji ya mto wa uzima". Tayari nimeshalionja joto la jiwe, nimekutana na upinzani mkubwa sana, nimeitwa muasi, niliepotea, nimerushiwa kila maneno ya laana. Lakini Mungu ajuae siri ya roho yangu amekua akinitia nguvu. Kuna wakati nilikata tamaa na kurudi nyuma na nilimwambia Yesu kwamba sitaweza kufanya utume alionipa kutokana na upinzani ninao upata, niliamua kurudi kwenye System (Taasisi) nilikokua natumika mwanzo. Nilimlilia sana Yesu nakumsii sana ampe mtu mwingine maono hayo, lakini Yesu akaniambia maneno haya "Ni wewe tu Amos ndie nimekuchagua ufanye kazi hii, nimekuandaa tangu ulipozaliwa, nimekutengeneza kwa kazi hii, nimekua pamoja nawe kila ulikokwenda, usiogope nitazame mimi utashinda. Peleka ujumbe kwa ndugu zako Rastafarian's (Marasta) na kwa Watoto wanaoishi mitaani, nitakupigania". Kwa machozi mengi niliamua  kuyabeba tena maono Yesu aliyonipa. Na tangu nilipoamua kufanya hivyo moyo wangu umekua na Amani. Nilienda tena mlimani kwenye msitu kufanya maombi, nikakaa siku 90 nikilala porini na kufanya maombi ya usiku na mchana. Malaika wa Mungu walinitokea marakadhaa na nimepata uthibitisho mkubwa kwamba mbingu yote iko pamoja nami. Ingawa mwili wangu umepungua sana kutokana na maombi ya kufunga kwa muda mrefu sana, lakini roho yangu imejaa moto mkali wenye uwezo wa kuchoma Dunia yote Amen!!!!!